Unaikumbuka ile stori ya kubuni ya mateja waliosubiri mwenzao aliyefuata kibiriti? Usijali hata kama hauikumbuki nitaisimulia kwa faida ya wengi. Mateja watatu walikuwa wakivuta bangi katika jumba moja lisiloisha(pagala), wakiwa wanaendelea na shughuli yao hiyo, wakagundua kuwa njiti zimewaishia. Hivyo wakamwagiza mwenzao mmoja ambaye naye tayari alikuwa "amesizi" akaombe kibiriti nyumba za jirani. Jamaa akatoka akaanza kuzunguka huku na huku. Akazunguka mpaka akazimaliza nyumba zote hakupata, mwisho akaingia katika jumba lile lile ambako wenzake wamo na akauza sera yake.
Jamaa: Dah, jamani samahani naomba mnisaidie kibiriti mara moja nikatumie nitarudisha. Wenzake wakajibu " Dah hata sisi kuna mshikaji tumemwagiza akatafute, kama vipi njoo tumsubiri". Kumbuka hapo anayesubiriwa ndio yule yule. Nilicheka sana siku ya kwanza ninasoma kisa hiki na nikachukulia ni mambo ya kufikirika. Kuna msemo mmoja maarufu "Chonde chonde, ulevi, nomaaa" sasa nauelewa sana. Dalili moja ya mtu kuwa katika ulevi uliopindukia ni kushindwa kujielewa na kufanya yasiyoeleweka. Naamini utakuwa umesikia na kushuhudia walevi wengi sana tangu ukiwa mtoto hadi sasa. Tofauti ni kuwa huwa wamelewa nini. Wengine ni walevi wa pombe, wengine walevi wa dawa za kulevya, wengine walevi wa kazi. Kiswahili kina maneno machache sana ya kuelezea ulevi. Kuna ulevi wa mambo mazuri , na ulevi wa mabaya, ambao unapaswa kuepukwa kabisa. Ninachoamini ulevi ni ulevi maana kila kitu kikifanywa kwa kuzidisha ni kibaya. Mtu anaweza kuingia katika ulevi aidha kwa kushawishiwa ama kwa kuamua mwenyewe. Ukishawishiwa ni mbaya zaidi maana unakuwa huna namna ya kujimudu, na bahati mbaya sana, mara nyingi wanaoshawishiwa huwa hawawezi kuacha maana wanaowazunguka ndio watumiaji na pia hawa wanaoshawishiwa huanza na ulevi wa kiwango cha juu sana. Kama ni pombe atakunywa zile kali kali, kama ni ngono atafanya mara nyingi sana kwa wiki. Aliyeshawishiwa kuingia kwenye ulevi, huwa inakuwa ngumu sana hata kumuelimisha juu ya ubaya wa suala hilo, labda pengine mpaka waliomshawishi waanze kubadilika na kuacha kabisa. Kitu kinachosikitisha kwenye ulevi ni kuwa mlevi huzingatia heshima na hadhi yake pale anapokuwa hajatumia, ila atakapotumia mfano kama ni pombe, si ajabu kumkuta hata mkurugenzi fulani akiwa ndani ya mtaro wa maji machafu na hashituki kuwa yuko pabaya. Unaweza kumuona mwalimu hata kama ni profesa anajisaidia barabarani na hazingatii kuwa pengine wanafunzi wake wanamuona. Yaani ulevi hupoteza heshima ya mtu. Humgeuza mkimya kuwa mpiga kelele na pengine mpiga kelele kuwa mkimya na tatizo la ulevi humfanya kimbaumbau kuwa baunsa.
Ukiacha watoto ambao wana miaka saba hadi kumi, hapa nchini kwetu, wengine tuliobaki asilimia zaidi ya 90% ya wapenda mpira, tumekua tukizipenda timu za Simba na Yanga. Inafika kipindi hata kocha wa timu fulani ambayo nayo inacheza ligi kuu lazima awe mshabiki wa Simba au Yanga. Nakumbuka siku moja, aliyekuwa nahodha wa timu ya taifa, Mecky Meksime alikuwa akihojiwa na mtangazaji wa televisheni fulani baada ya kuwa amestaafu na kukabidhiwa mikoba ya kuinoa Mtibwa Sugar. Mtangazaji akamuuliza "Wewe ni shabiki wa Yanga au Simba". Mecky akacheka kidogo na kusema kuwa yeye hana timu kati ya hizo, yeye ni mshabiki wa Mtibwa Sugar. Mtangazaji hakutaka kuamini hilo. Akandelea kusisitiza kuwa hata kama ni mshabiki wa Mtibwa lazima ana timu kati ya hizi mbili. Sikumshangaa na wala sitamlaumu mtangazaji yule kwa kuwa ndivyo alivyoamini na mara nyingi hali ilikuwa hivyo. Utawala wa Simba na Yanga ulikuwa umemeza timu nyingine nyingi kipindi kile. Hata kwenye mbio za ubingwa hizi ndio zilikuwa zinatawala, vilikuwa vibaba viwili vinapigania mke, huyu akichukua leo yule anachukua kesho. Mchezaji sijui wa Kahama United, sijui Majimaji au Ashanti akionekana mahiri tu, msimu ujao anatua Simba au Yanga. Hali hii ikapelekea hawa jamaa kujiona kuwa hakuna wa kuwazuia maana hata viongozi wa TFF/ FAT walikuwa ni wanachama wa vilabu hivi nguli( japo hili hadi leo) haikuwa inazuiliwa kiongozi kuwa mshabiki wa chama na hata leo haizuiliwi lakini pale mapenzi ya klabu yanpoongoza kuliko weledi ni kasoro(ulevi). Kwa kifupi mpira wetu wote ulikuwa Simba Yanga. Enzi hizo hata ukienda kuangalia mechi ya Taifa stars utasikia watu wanashangilia kulingana na timu zao, kumbuka timu ya taifa ilikuwa ina wachezaji wa vilabu viwili tu. Hivyo akifunga wa Yanga, mashabiki wa Yanga watashangilia, akifunga wa Simba watashangilia mashabiki wa Simba pekee yao. Hali kadhalika akiharibu mchezaji wa Yanga wa Simba watazomea na Yanga vivyo hivyo anapoharibu wa Simba. Mtu aliyemo kwenye mfumo huo wa ulevi alikuwa anashindwa kuliona hilo.
Mwaka 2008, kidogo hali ikabadilika. Azam Footbal club, walipanda daraja na kuingia ligi kuu. Mvuto wa kipekee ulijengeka maana timu hiyo kwanza ilikuwa timu ya kwanza inayomilikiwa na mtu binafsi kupanda ligi kuu. Pili ule u mwamba wa Bakhresa katika biashara ulikuwa unaleta uvuvio mpya katika soka la Tanzania, kingine ni kuwa Azam ilipanda daraja bila kucheza ligi moja misimu miwili. Yaani walicheza dara la nne msimu mmoja, la tatu msimu mmoja, la pili na la kwanza hivyo hivyo na wakapanda ligi kuu. Kwa muda pale, u simba na u yanga ulitiwa giza. Hata taswira ya timu ya taifa nayo baada ya muda mfupi ikaanza kupambwa na akina Bocco wa Azam. Nikawa najihoji sasa ikishuka daraja itakuwaje? Aah haikuwa hivyo, Azam wakawa wanapigania nafasi za juu. Azam wakanithibitisha ubora wao pale walipokuwa wanatengeneza vijana wazuri sana hasa katika eneo la kiungo. Azam ikawa tamu kama ice cream zao. Yule mzee Bakhresa akaamua kuonesha wapi tulikwama tulipokuwa tunavaa jezi za njano na kijani au nyekundu na nyeupe. Akaamua kujenga "facility" za timu pale chamazi. Uwanja wa kisasa, mabwawa ya kuogelea, gym, hostel na ofisi vyote katika sehemu moja. Akatupa sababu ya kutafuta jezi za bluu. Wakamwita Abramovic wa Tanzania. Nikawa na furaha moyoni kuwa timu zetu kubwa zitajifunza kuwa na mfumo bora zaidi wa timu za vijana, kuwa na makao makuu bora ya timu na zaidi kuwa na mfumo bora wa uongozi. Furaha ikazidi pale walipochukua ubingwa wa ligi kuu. Nikaona huu ndo mwanzo bora wa kesho nzuri. Kwa kifupi ni kuwa Azam alileta mapinduzi ya soka hapa kwetu.
Maumivuuu, hali haiko hivyo kwa sasa. Yaani tunakoelekea tunarudi kwenye zama zetu zileee. Tofauti yake tu kwa sasa ni kuwa kutakuwa na wakubwa watatu. Simba, Yanga na Azam. Kwa maana nyingine wawili wa kariakoo ama wakongwe na mmoja wa Chamazi. Wakongwe ni wazoefu katika masuala ya ujanja ujanja katika ligi. Wanajipangia marefa, wanarubuni wachezaji wa timu pinzani ama walioko nje ya nchi, wanarubuni makocha, hawakosi sababu kila wanapofungwa na mara nyingi sababu zao lazima mtu alaumiwe. Azam naye amekwisha kinywea kikombe cha wakongwe wa Kariakoo. Sasa hivi utasikia Azam anahusishwa na skendo ya kupanga marefa, anatoa sababu za lawama pale anapopoteza mchezo, anapata safari ya kwenda nje katikati ya ligi kucheza bonanza anakwenda, hataki kuuza wachezaji wa kiTanzania nje ya nchi kwa kuwarubuni kimtindo. Hahaha yaani tumekaa tunasubiri jamaa akalete kibiriti na mleta kibiriti naye amekaa anasubiri. Ulevi nomaa. Kwa waliyokuwa wameyafanya Azam nilitegemea wangeendelea kuwa mfano na kuwaburuza wakongwe katika mpira huu, kuanzia kiuongozi hadi kimchezo na kimataifa lakini wamekwama nao. Juzi katika mechi ya Azam na Panone namsikia kocha wa Azam anasema "This is a pitch for goats" yaani " Huu ni uwanja wa mbuzi" sio uwanja wa kucheza binadamu wanapaswa kucheza mbuzi. Kidogo niliona ni sababu ya maneno. Uwanja wa ushirika naamin ni maoni ya kwanza kusikia ukisemwa ni uwanja wa mbuzi. Azam wameangukia kwenye mtego ule ule wa wakongwe, nao wanahusishwa na dili za upangaji wa ratiba, upangaji wa marefa na kuhujumu wachezaji. Hadi sasa tunapoongea sijasikia Azam wakiuza mchezaji kwenda nje ya nchi, hasa MTanzania. Cha zaidi ambacho nimepata kusikia ni skendo kuwa waliwarubuni baadhi ya wachezaji waliopata nafasi ya kufanya majaribio ulaya ama nje ya Tanzania kwa kuwapa magari mazuri, kuwaongezea mishahara na kuwawekea vizuizi vya kiuongozi. Sio mabaya kuwalipa vizuri wachezaji lakini kwa maslahi ya Taifa mchezaji anahitaji kupata jukwaa bora zaidi kwa ajili ya kuongeza kiwango, tofauti na ligi ya hapa ndani. Maana kama Azam angekuwa na uwezo wa kuwatumia vyema wachezaji hawa angalau angethibitisha kwa kufika mbali michezo ya kimataifa. Siku baada ya siku Azam inazidi kuwa ya "Kitanzania", sio ya kisasa tena.
Bado hamjachelewa, mnisamehe kama nakosea, lakini ninapenda nishuhudie mapinduzi ya kisoka na mwanga wa hilo hapa nchini, mnao ninyi. Mmekuwa wa kwanza kwenye mambo mengi sana. Iko wapi furaha mliyonipa kwa kutwaa ubingwa wa ligi kuu? Yako wapi matarajio makubwa mliyoniandaa kuyapokea pale mlipojenga uwanja wenu Chamazi? Uwanja ambao hata hivyo hamjawahi kuutumia kwa mechi za Simba na Yanga. Uko wapi mshangao mlionipa kwa kuwapa nyumba wachezaji wenu wote? Ziko wapi sifa nilizowapa kwa kuleta basi la kisasa la wachezaji? Ulimwegu wa wanasoka unatamani kuendelea kushuhudia mambo makubwa kutoka kwenu. Cha ajabu ni haya madoa ambayo mnapakwa na matukio ambayo yanawafanya muonekane kufanana na wakongwe. Ndio, wakongwe wale wa Kariakoo. Mmoja msimbazi mwingine Jangwani. Wale ndio tumezoea kuona wakihusishwa na migogoro na skendo za kila aina kila wakati. Mwaka huu Simba wakitulia, ujue Yanga kutazuka tatizo, Yanga nao wakitulia linaibukia msimbazi mpaka ninaamini kuwa kule kuna pombe ya aina moja wanayoitumia, naam, pombe ya Kariakoo. Cha kuzingatia sana ni kuwa ukimwamsha aliyelala utalala wewe, simba wamefungua duka rasmi la vifaa na bidhaa za timu, mbeya City wana bidhaa za timu kila kona lakini ninyi waamshaji mnarudi kule. Kwa uongozi wa Azam ulivyo sikutegemea haya yatokee. Na hapo ndio ninapatwa na wasi wasi hadi najiuliza, Azam, mmelewa pombe ya Kariakoo??
GULINJA EZEKIEL GASPER
IG & TWITTER: dc_gitaa
Whatsapp: 0766562588
©Gitaa Inc.